Virusi vya HIV vyaanza kujenga kinga


Virusi vya HIV
Virusi vya ugonjwa wa ukimwi vinaendelea kujenga kinga dhidi ya dawa za ugonjwa huo zinazotumika kukinga na kukabiliana na ugonjwa huo,utafiti umesema.
Virusi vya HIV vimeanza kuwa na kinga dhidi ya dawa ya Tenovir katika asilimia 60 ya visa vyote miongoni mwa mataifa kadhaa ya Afrika kulingana na utafiti huo uliofanyika kati ya mwaka 1998 na 2015.

Utafiti huo ,ulioongozwa na chuo kikuu cha London,uliwashirikisha takriban watu 2000 walio na virusi hivyo duniani.
Kiongozi wa utafiti huo Daktari Ravi Gupta amesema kuwa matokeo yake yalizua wasiwasi mkubwa.
Kazi hiyo iliochukua miaka minne kukamilisha.Ilianza mwaka 2012 na iliwalinganisha wagonjwa wa ugonjwa huo barani Afrika na wale wanaoishi barani Ulaya.
Huku wagonjwa hao wakigawanywa katika makundi mawili,utafiti huo ulibaini kwamba barani Afrika asilimia 60 ya wagonjwa walikuwa hawatibiki na dawa ya Tenovir huku barani Ulaya idadi hiyo ikipungua na kuwa asilimia 20.

 Dawa za ukimwi
Matokeo hayo ambayo yamechapishwa katika jarida la Lancet kuhusu magonjwa ya maambukizi,ulisema kuwa usimamizi m'baya wa dawa hizo kama vile kutozitumia zinavyohitajika na katika viwango vilivyo sawa huenda ndio sababu ya tatizo hilo.
''Iwapo viwango sawa vya dawa hiyo havitatumika ,virusi vinaweza kukabili dawa hiyo na kuwa na kinga'',Daktari Gupta aliiambia BBC.
''Tenovir ni dawa muhimu katika vita dhidi ya virusi vya ukimwi,kwa hivyo inatia wasiwasi sana kuona viwango vya virusi vilivyo na kinga dhidi ya dawa hiyo'',aliongezea.
Utafiti huo pia umesema kuwa virusi vilivyo na kinga dhidi ya Tenovir vinaweza kusambazwa kutoka kwa mtu mmoja hadi mwengine.